KAWEGERE, MWANDISHI
WA ‘SHAMBA LA WANYAMA’ BADO ANATETEA
HAKI
Na Hezekiel Gikambi
akiwa Bukoba, Tanzania, Agosti 2013
Katika Kongamano la hivi majuzi la kumbukumbu la miaka 50 la kumuenzi mwandishi mashuhuri wa riwaya na mashairi marehemu Sheikh Shaaban Suleiman Ufukwe Bin Roberts almaarufu Shaaban
Roberts mjini Bukoba Tanzania, nilikutana na
mwandishi mwengine maarufu sana. Huyu si mwingine bali ni Bw.Fortunatus Felix
Kawegere aliyetafsiri na kuifasiri riwaya iliyoibukia kupendwa sana ya Shamba
la Wanyama kutoka kwa riwaya asilia ya Mrusi George Orwell ya Animal Farm.
Wasomaji wa kazi zako hasa riwaya maarufu Shamba la Wanyama wangependa kukufahamu
zaidi.
Nilizaliwa tarehe
08/04/1943 hapa mjini Bukoba mkoani Kagera nchini Tanzania na kusomea katika
shule ya Msingi ya Bunena baina ya mwaka wa 1950- 1954 na kuendelea na Shule ya
Kati ya Kitejagwa –kama ilivyoitwa enzi hizo. Baadaye nilijiunga na Chuo cha
Ualimu cha Kijunguti baina ya mwaka wa 1960-1961. Tarehe hiyo inakuambia kuwa
nilikamilisha kozi ya ualimu wakati Tanganyika inapata uhuru wake.
Masomo yako yalikomea hapo au ulijiendeleza zaidi?
Niliamua kupiga hatua
mwenyewe kimasomo kwa kujisajili na vyuo vilivyotoa masomo kwa njia ya posta
vilivyoitwa ‘Rapid Results’ kati ya mwaka 1960-1963. Nilichukua somo la Lugha
ya Kiswahili, Uchumi na Biashara. Kwa kweli nilimakinikia somo la Kiswahili kwa
kuwa nimekuwa nikiipenda sana lugha hii. Napenda chochote kinachomtambulisha
mtu yeyote na kukuza utamaduni wake. Hapo ndipo mbegu ya uandishi ilipoatikwa
na ikamea na kuzidi kupaliliwa na mapenzi yangu kwa Kiswahili.
Ulianza lini kazi ya uandishi
wako na uliiendelezaje?
Nilisoma riwaya ya
George Orwell ya Animal farm mwaka wa 1964 na ikanichochea sana. Niliona kama
inamulika na kuakisi uhalisia katika jamii yetu kwa kiwango kikubwa mno.
Nilipata mshawasha wa kuifasiri riwaya hiyo kwa Kiswahili mwaka wa 1965 ili
ujumbe uliokuwemo uwafikie wananchi wa Tanganyika na Afrika Mashariki kwa jumla.
Kilichapishwa mwaka wa 1967. Kabla ya
hapo nilikuwa tayari nimeandika riwaya ya Kiingereza ya upelelezi iitwayo-Inspector Rajabu investigates. Nilipokuwa
Mwalimu, Wizara ya Elimu pia iliniita Chuo cha Walimu cha Kiburunyembe,
Morogoro kushiriki katika kuandika
kitabu cha wizara cha kozi ya mafunzo ya Kiswahili kilichoitwa Tujifunze Lugha
Yetu. Sura tatu nilizoandika kama vile Gulio la Katerero, Mbunge wetu, ziliibukia
kupendwa sana. Hapo nikajitoza kikamilifu katika uandishi. Nimeandika vitabu vingine kama vile riwaya ya
Kinga ya Rushwa, diwani ya Mashairi ya Kazi yangu, Uongo uliozaa jitu, Sayari iliyozama,
Mgeni wa Usiku na vya Kiingereza kama
Flying without Wings, A Narrow Escape na A Dancing Boat. Ninaendelea kuandika.
Serikali changa ya Tanganyika ilichukuliaje riwaya ya Shamba
la Wanyama inayosawiri viongozi wanaowadhulumu raia wake?
Kwa sadfa kubwa,
riwaya ya Shamba la Wanyama ilipotoka mwaka wa 1967, ndipo Azimio la Arusha
lilipopitishwa na kuzinduliwa rasmi. Azimio
hilo lilikuwa kama ramani ya taifa. Nilikuwa na mgogoro kidogo na
utawala kwa kuwa labda serikali ya Mwalimu Julius Nyerere ilifikiria kuwa
kitabu changu kitapingana na mfumo wetu mpya wa Ujamaa. Walinijia maafisa wa
polisi na vijana wa usalama wa taifa na kunihoji wakitaka kujua madhumuni yangu
katika kutoa kitabu cha ‘kisiasa’. Niliwajuza kuwa hata sikuwa na habari kuwa azimio
la azimio lipo au litatoka lini? Viongozi wengi serikalini hawakukipenda sana
kwa kuwa
Mbona kazi zako nyingi zinaelekea kutetea haki za umma na
kupinga dhuluma katika jamii?
Kwa kweli mimi
napenda siasa sana. Nimewahi kuwa diwani wa Manispaa ya Bukoba miaka ya 1980 na
hata baadaye nikajaribu kugombea ubunge ila nikaibuka wa tatu mwakani 1985. Sidhani
hadi wa sasa kama nilishindwa kihalali. Ninaona siasa kama njia moja ya kutoa
uongozi na kuelekeza jamii na kufikia hadhira kubwa. Siasa sasa zimegeuzwa jukwaa
la kujichumia mali kwa urahisi. Hata nimeangazia dhuluma katika jamii katika kazi zangu kama ‘Sayari iliyozama’ ambapo
nilitumia ndege kuonyesha uozo wa kimaadili kama ulaji rushwa na wizi wa kura uchaguzini na kadhalika. Mathalan,
riwaya ya Shamba la Wanyama ni kioo cha uhalisia ulioko katika serikali zetu
hasa barani Afrika ambapo viongozi wanaanza kwa lengo moja la kupinga dhuluma
lakini hatimaye wakishatwaa hatamu za uongozi, wanabadilika na kuwa kama watangulizi wao. Yule mhusika
nguruwe aliyeitwa Mkimwa riwayani na wengineo kwa mfano ni viwakilisho hakika
vya viongozi kama hawa.
Riwaya ya Shamba la Wanyama ilisomwa sana Kenya au Tanzania?
Kusema ukweli,
kilishamiri sana nchini Kenya kuliko hapa Tanzania. Mauzo yake hadi wa sasa
nchini Kenya ni ya kufurahisha. Kimekuwa kikisomwa kama riwaya teule nchini
Kenya kwa miaka mingi. Labda ni kwa sababu palitoa mwamko mpya wa kisiasa na
kijamii nchini Kenya kabla ya Tanzania kwa kuwa sisi hapa tulilimatia katika siasa
za kujitegemea za Ujamaa. Utamaduni wa kusoma ulikita mizizi Kenya kuliko
Tanzania.
Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alikuathiri kwa njia yoyote
katika uandishi wa wako?
Mwanzo mimi nilishuhudia Tanganyika ikijinyakulia uhuru.
Zile hotuba za Mwalimu Nyerere za kwanza na mwelekeo tuliokuwa tumeanza nao
ulikuwa unatia moyo sana. Kidogo kidogo
tulianza kupoteza mwelekeo na lengo tuliloanza nalo. Niliposoma Animal Farm ya George Orwell nikaanza
kung’amua kuwa kumbe haya ninayoyasoma
riwayani inaelekea ni kama yanayoanza kutokea nchini. Hilo likanisukuma
kuharakisha kukitoa kitabu hiki. Pia uhalisia wa mambo nchini Tanzania wakati
huo ulinisaidia kutafuta majina ya wahusika katika Kiswahili.
Je, bara la Afrika katika karne ya 21 limetoka katika ‘Shamba
la Wanyama’?
Kwa maoni yangu, hata hali ni mbaya zaidi katika nchi zetu
kwa kuwa pengo baina ya tabaka la maskini na matajiri linazidi kupanuka.
Viongozi wanaboresha maslahi yao ni kusahau ya umma. Tunashuhudia wabunge wetu
wakijiongeza posho na hata mishahara wakati walimu hawalipwe hela zao. Kama
nguruwe kina Mkimwa walivyojiongeza maziwa, wanasiasa wanajijaji tu. Uzuri wa
mambo ni kuwa kuna demokrasia na uhuru wa kujieleza kuliko siku za mwanzoni.
Suluhisho lipo katika kizazi kipya kikipewa nafasi za uongozi . Wafike mahali
na wakatae hongo na uozo wowote katika jamii na wajitenge na Waliotangulia.
Waandishi kama wewe watabadilishaje jamii na kuiboresha?
Kazi za fasihi zina
nafasi kubwa ila pia kuna changamoto kwa kuwa utamaduni na hamu ya kupenda
kusoma kazi hizo ili wapate ujumbe. Vipo vitabu vingi vilivyo na ujumbe
unaoweza kubadilisha hata mifumo ya kisiasa. Tumejitolea hata kupunguza hata
bei za vitabu ili viingie shuleni lakini mwitiko ni mdogo sana. Unashangaa
wanafunzi wanaanguka mtihani kwa asilia kubwa kwa kukosa kusoma. Pia mifumo ya
elimu inahitaji mabadiliko. Wizara ya elimu ina jukumu la kuwaridhirisha walimu
na kutoa mitalaa inayoambatana na maendeleo katika jamii. Vitabu sibakia kama
biashara tu.
Sasa unajishughulisha na nini?
Mimi bado nazidi
kuandika vitabu. Hivi karibuni nitatoa tamthilia yangu. Aidha ninafanya kilimo
katika shamba langu pamoja na ufugaji. Hali kadhalika ninatoa mchango wangu
katika jamii ya Bukoba kama mjumbe wa Baraza la Ardhi na Nyumba nikiwa mmoja wa
washauri. Pia mimi mwenyekiti wa chama
cha SACCO ya kata ya Kibeta na vikundi vinginevyo. Pia ninashiriki katika
shughuli za UKUTA kama Katibu wake. Ukuta ni Chama cha Usanifu wa Kiswahili na
Ushairi -UKUTA- ambacho kimeshirikiana na BAKITA-Baraza la Kiswahili la Taifa
na Taasisi ya Taaluma za Kiswahili- Chuo Kikuu cha Dar es Salaam-TATAKI katika
kuandaa hafla hii ya kumuenzi Shaaban Roberts.
Hezekiel Gikambi ni mtaalamu
wa lugha ya Kiswahili na Tafsiri na pia Meneja wa Mradi wa Swahilihub.com wa
Nation Media Group, Nairobi Kenya na mwandishi wa Safari ya Serengeti.
Barua pepe: hezekielgikambi@gmail.com

No comments:
Post a Comment